Isaiah 15

Unabii Dhidi Ya Moabu

1 aNeno kuhusu Moabu: Ari iliyo Moabu imeangamizwa:
imeharibiwa kwa usiku mmoja!
Kiri iliyo Moabu imeangamizwa,
imeharibiwa kwa usiku mmoja!

2 bDiboni anakwea hadi kwenye hekalu lake,
mpaka mahali pake pa juu ili walie,
Moabu anaombolezea Nebo na Medeba.
Kila kichwa kimenyolewa
na kila ndevu limeondolewa.

3 cWamevaa nguo za magunia barabarani,
juu ya mapaa na kwenye viwanja
wote wanaomboleza,
wamelala kifudifudi kwa kulia.

4 dHeshboni na Eleale wanalia,
sauti zao zinasikika hadi Yahazi.
Kwa hiyo watu wenye silaha wa Moabu wanapiga kelele,
nayo mioyo yao imezimia.


5 eMoyo wangu unamlilia Moabu;
wakimbizi wake wanakimbilia Soari,
hadi Eglath-Shelishiya.
Wanapanda njia ya kwenda Luhithi,
wanakwenda huku wanalia;
barabarani iendayo Horonaimu
wanaombolezea maangamizi yao.

6 fMaji ya Nimrimu yamekauka
na majani yamenyauka;
mimea imekauka wala hakuna
kitu chochote kibichi kilichobaki.

7 gKwa hiyo mali waliyoipata na kujiwekea akiba
wamezichukua na kuvuka Bonde la Mierebi.

8 hMwangwi wa kilio chao umefika hadi mpakani mwa Moabu,
kilio chao cha huzuni kimefika hadi Eglaimu,
maombolezo yao hadi Beer-Elimu.

9 iMaji ya Dimoni yamejaa damu,
lakini bado nitaleta pigo jingine juu ya Dimoni:
simba juu ya wakimbizi wa Moabu
na juu ya wale wanaobaki katika nchi.
Copyright information for SwhKC